Pages

CONTACT

0757092504/0678321772

Thursday, October 30, 2014

MHE. PINDI H. CHANA: KATIBA IMEZINGATIA HAKI ZA WATOTO




 



Na Erasto Ching’oro - Msemaji Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Mhe. Pindi H. Chana akiwasilisha Taarifa ya Nchi Kuhusu Hali ya Maendeleo ya Wanawake, Ulinzi na Maendeleo ya Watoto kwenye Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa uliofanyika New York Marekani, tarehe 17/10/2014.



Naibu waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Mhe. Pindi Chana (Mb.)amepongeza Bunge la Katiba kwa kuzingatia haki za msingi za watoto katika mapendekezo ya Rasimu ya Katiba ya nchi kwa kujumuisha Ibara Na. 53 (1) – (3) inayohusu haki za watoto nchini. 

Taarifa ya Sensa ya Taifa ya Idadi ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, inaonyesha kuwa, Tanzania Bara ilikuwa na watoto 21,866,258 wenye umri wa chini ya miaka 18 ambao ni sawa na asilimia 51 ya watu wote. Hata hivyo kundi hili lina changamoto mbalimbali za upatikanaji wa huduma za malezi, mkuzi na maendeleo ya mtoto. 

Mhe. Pinda ametanabaisha kuwa, kukosekana kwa huduma hizi husababisha vifo, ukatili, ongezeko la watoto wa mazingira hatarishi, mmomonyoko wa maadili, unyanyapaa kwa watoto wenye mahitaji maalum, ukeketaji, na ndoa za utotoni. 

 Kero hizi zinahitaji jitihada tahbiti madhubuti ili kuhakikisha watoto wanapata haki zao za msingi. 

Mhe. Chana anabainisha kuwa, kwa sasa suala la haki za watoto limezingatiwa katika rasimu ya Katiba ya nchi inayopendekezwa, kwa kupatiwa sura kamili namba 53.

 Lengo kuu la Serikali likiwa ni kuhakikishwa kuwa haki za msingi za watoto zinatekelezwa kikamilifu ikiwa ni pamoja na haki ya kuishi, kulidwa, kuendelezwa, kushirikishwa, na kutobaguliwa.

Kwa mujibu wa Ibara Na. 53 (3) ya Rasimu ya Katiba, mtoto anatambuliwa kama mtu mwenye umri wa chini ya miaka kumi na nane.
 Akizungumza wakati akitoa majumuisho ya ziara yake ya kutembelea vituo vya kulelea watoto, jijini Dar es salaam, Mhe. Pindi Chana amepongeza Bunge la Katiba kwa kupendekeza Ibara Na. 53 ambayo inawataka wadau wa haki za  mtoto kuwa na mikakati jumuishi itakayo hakikisha kuwa mtoto anapata jina, na uraia wa kusajiliwa. 


Tafiti zinaonyesha kuwa, kiasi cha asilimia 14 tu ya watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano hapa nchini ndio waliokuwa wamesajiliwa na asilimia 6.2 ya watoto wote nchini waliokuwa na vyeti vya kuzaliwa.

 Kwa vile suala hili ni moja ya agenda ya watoto, limeingizwa katika katiba ya nchi ili kuongeza uwajibikaji miongoni mwa watoa huduma za ulinzi kwa ajili ya uimarishaji wa maslahi ya watoto ikiwemo haki ya uraia na kuusajiliwa.

Pindi Chana ameongeza kuwa ibara Na.53 (b) ya Katiba ya nchi imezingatia haki ya watoto kutoa mawazo yao, kusikilizwa na kulindwa dhidi ya uonevu, ukatili, udhalilishaji, na utumikishwaji na inapinga madhara yanayotokana na mila potofu. 

Kundi hili ni kubwa hivyo linahitaji uangalizi makini katika malezi, makuzi na maendeleo yao ili hatimaye kuwa na raia wema walioandaliwa na kuwa na mchango thabiti katika familia zao na taifa kwa ujumla.

Watoto na wananchi kwa ujumla wanakumbushwa kutoa taarifa za vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa watoto, ili wanaoendeleza uaktili dhidi ya watoto waweze kuchukuliwa hatua stahiki. Taarifa hizo zinaweza kutolewa kupitia kwa maafisa wa madawati ya jinsia, Namba maalum ya msaada wa mawasiliano kwa watoto na. 116, walinzi wa amani walio karibu, wadau wa ulinzi wa watoto na Wizara yenye dhamana kwa Watoto, na raia wenye mapenzi mema kwa watoto.

 Wizara yenye dhamana kwa masuala ya watoto itaendelea kuratibu utoajai wa elimu na uhamasishaji wa wadau mbalimbali kuhakiksha kuwa jamii inashiriki kuwalinda watoto katika ngazi zote. 

Rasimu ya Katiba imependekeza kuhusu kuwawekea watoto mazingira bora ya kucheza na kupata elimu ya msingi. 

Serikali inatambua kuwa katika hatua za awali za mtoto, huduma za uchangamshi wa awali na michezo ni  muhimu kwa ajili ya kujenga upeo wa uelewa wa mtoto. 

Hili ni pamoja na kujifunza, kuelekezwa mambo mbalimbali, kuimba, kucheza na kufanya mazoezi ya vitendo vya uchangamshi. Katiba inazingatia kuwa, katika umri wa chini ya miaka 18 watoto wanahitaji kupatiwa elimu bora na kutambuliwa na kuendelezwa vipaji vyao tangu hatua ya awali.

 Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa ushirikiano na wadau ili kuona kuwa maslahi ya watoto wanafikiwa katika utimilifu wake.

Sura ya 53(e) ya Rasimu ya Katiba inapendekeza mtoto kupata lishe bora, huduma ya afya, makazi na mazingira yanayomjenga kimwili, kiakili na kimaadili.

 Tafiti zinaonyesha kuwa asilimia 58 tu ya kaya nchini ndizo zinauwezo wa kununua chakula na asilimia 6 zinategemea msaada ili ziweze kupata chakula (USAID; 2011).

 Hali hii inaathiri upatikanaji wa lishe bora na hivyo kurudisha nyuma huduma ya malezi, makuzi na maendeleo ya mtoto hususan katika umri wa miaka 0 - 8. Kuingizwa kwa kifungu hiki kitatoa msukumo katika uzingatiaji wa lishe kwa watoto. 

Mhe. Chana amefafanua kuwa, Sura 53(e) inahimiza utoaji wa huduma ya afya kwa mtoto kwani haki ya kuishi inaanza pale mama anapopata ujauzito. 

Vile vile, kuishi kwa watoto baada ya kuzaliwa kunategemea upatikanaji wa chakula cha kutosha, huduma bora za afya na ulinzi katika kuhakikisha mtoto anakuwa na afya ya kutosha kumwezesha kukua na kufikia ndoto zake.

 Kupatikana kwa huduma hii katika mfumo jumuishi kutamwezesha mtoto kuwa salama katika nyanja zote za malezi na makuzi yake. 

Vile vile, kifungu hicho kimeeleza kuhusu huduma ya makazi na mazingira yanayomjenga mtoto kimwili, kiakili na kimaadili. Naibu Waziri Chana anasema kuwa, tatizo la ukosefu wa maji na uchafu  wa mazingira lipo katika maeneo ya kuelea watoto, shule, na makazi yetu.

 Hali hii inakwamisha juhudi za taifa katika utoaji wa huduma za malezi, makuzi na maendeleo ya mtoto. 

Kuhusu ushiriki wa watoto, Rasimu ya Katiba inapendekeza mtoto kushiriki katika shughuli zinazolingana na umri alionao kama inavyoelezwa katika sehemu ya 53(e).

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto inatambua kuwa maendeleo ya ukuaji wa mtoto hutegemea ushiriki wake katika masuala yanayomuhusu na yale yanayohusu jamii kwa ujumla.

 Hali hii humwezesha mtoto kutoa mchango katika maamuzi yanayohusu maendeleo yake na yale yanayo paswa kutekelezwa na jamii.

Hatua za ushiriki wa mtoto zinaanzia umri wa miaka mitatu hadi anapokuwa mtu mzima ambapo aina ya masuala anayopaswa kushirikishwa hutegemea umri wake.

 Misingi hii ya ushiriki, imeelekezwa katika mikataba ya kimataifa ya haki za watoto, katiba, sheria na kanuni mbalimbali.

 Wizara ya maendeleo ya jamii, Jinsia na Watoto imetoa maelekezo ya kuundwa mabaraza ya watoto kama hatua moja ya kuimarisha ushiriki wa watoto katika ngazi mbalimbali za kijamii.

 Kwa kutambua hili, kuna umuhimu mkubwa wa kuelimisha wazazi na jamii kukuza uelewa kuhusu ushirikishwaji wa watoto katika masula mbalimbali ili kukuza maslahi ya watoto na viwango vya utoaji huduma stahiki kwa watoto wetu. 

Halikadharika, kifungu 53(g) kinapendekeza mtoto kupata malezi na ulinzi kutoka kwa wazazi, walezi, jamii au mamlaka ya nchi, bila ya ubaguzi wowote. 

Ubaguzi ambao umeripotiwa ni ule wa kijinsia ambao mtoto wa kike au wa kiume anabaguliwa na wazazi au jamii; na ule unaotokana na hali ya ugongwa, ulemavu na uyatima. Wizara na wadau wake wamekuwa wakielimisha jamii kuhusu madhara ya ubaguzi wa watoto.

 Hata hivyo bado kuna taarifa za watoto wanaowabaguliwa kwa sababu moja au nyingine jambo ambalo Mhe. Pinda Chana analikemea vikali kwani lina madhara makubwa kwa watoto kisaikolojia na kiakili.

Mhe. Pindi Chana anahitimisha kwa kubainisha kuwa, mapendekezo ya Rasimu ya Katiba yameelekeza kuwa, ni wajibu wa kila mzazi, mlezi, jamii na mamlaka ya nchi kuhakikisha kuwa watoto wanalelewa katika maadili stahiki kwa umri wao.

 Kama agizo hili likifanyiwa kazi na kusimamiwa na walinzi wa watoto, tutapunguza kwa kiasi kikubwa matukio ya uaktili kwa watoto na kuwa na taifa la watoto na vijana makini walioandaliwa kubeba dhamana katika familia na taifa kwa ujumla. 
 
Kimsingi, uwezo wa taifa lolote lile kwa kiwango kikubwa unategemea ni kwa kiasi gani maslahi ya watoto yamezingatiwa kwa kuwekeza katika malezi, makuzi na maendeleo ya mtoto. 

Kushindwa kutoa kipaumbele katika upatikanaji wa haki za watoto kutaongeza athari mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa ukatili, vifo katika umri mdogo, utoro shuleni, mimba za utotoni, watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, ajira hatarishi na hivyo kuongeza gharama kwa familia na taifa letu. Taifa ambalo limezingatia ulinzi na uwekezaji katika maslahi ya watoto linakuwa taifa thabiti maana liliandaa mustakari wa watoto wake kwa wakati unaofaa. 
 

Simu: 0715496900

No comments:

Post a Comment