Pages

CONTACT

0757092504/0678321772

Friday, May 29, 2015


MFANYABIASHARA wa jijini Dar es Salaam, Brayan Kikoti ameonesha nia ya kuwania ubunge katika jimbo la Kilolo linaloongozwa na Profesa Peter Msolla.
 
Akizungumza na wanahabari mjini Iringa hivi karibuni, Kikoto anayesoma Diploma ya Juu ya Utatuzi wa Migogoro katika Chuo cha Ustawi wa Jamii, jijini Dar es Salaam alisema atawania jimbo hilo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
 
Endapo atapitishwa, alisema atahakikisha wananchi wa jimbo hilo wanakabiliana na umasikini kwa kutumia ardhi nzuri waliyonayo.
 
“Kilolo ina ardhi nzuri na hali ya hewa nzuri. Inahitaji kiongozi atakayewasaidia wananchi wa jimbo hilo namna ya kuitumia rasilimali hiyo kubadili maisha yao nay a Taifa kwa ujumla,” alisema.
 
Alisema wana Kilolo wanatakiwa kukaa upya na kuangalia kwa kina namna walivyoteleza na kuigawa ardhi yao kwa wawekezaji wa miti.
 
“Wapo baadhi ya wananchi waliouza ardhi yao kwa bei chee kwa wawekezaji hao na leo wanatafuta vipande vya ardhi kwa ajili ya shughuli zao zingine lakini hawapati; tutapitia upya makubaliano ya uuzaji wa ardhi kwa wawekezaji hao ili tuone kama kulikuwa na udanganyifu tuweze kuufanyia kazi kwa faida ya wananchi,” alisema.
 
Kikoti alisema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wanaofanya biashara zao Machinga Complex jijini Dar es Salaam amewahi kuwa msaidizi wa mbunge wa Wawi, Hamda Rashid alipokuwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
 
Ni mtoto wa nane kati ya tisa wa Mzee Kikoti na Paulina Luhwago; alizaliwa katika kijiji cha Ng’ing’ula alikopata elimu yake ya msingi kabla ya kujiunga na elimu ya sekondari katika shule ya sekondari Udzungwa na baadaye kusoma kozi ya kompyuta jijini Nairobi.
Baada ya kumaliza kozi hiyo ya kompyuta, Kikoti alijiunga na Chuo cha Ualimu Morogoro kabla hajajiunga kwa kozi nyingine ya Diploma ya Kufundisha Watoto wadogo. Baada ya kuhitimu mafunzo hayo alijikita katika biashara zikiwemo za Utalii anazoendelea nazo mpaka sasa.


No comments:

Post a Comment