Pages

CONTACT

0757092504/0678321772

Thursday, August 6, 2015

RAIS KIKWETE AAGA WATUMISHI WA MAHAKAMA KUU

download (9)
Na Lilian Lundo, Maelezo
Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wampongeza Mhe. Rais Dokta Jakaya  Kikwete, kitendo cha  kuheshimu Katiba ya Nchi, Utawala wa Sheria na uhuru wa mahakama.
Pongenzi hizo zimetolewa leo na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman wakati wa hafla ya mahakama hiyo ya kumwuaga Rais Kikwete iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Akisoma taarifa ya maendeleo ya mahakama kwa kipindi cha miaka kumi ya Serikali ya Awamu ya Nne, Jaji Mkuu alisema Rais Kikwete  alipoingia madarakani mwaka 2005, kiwango cha fedha kilichokuwa kimetengewa na Serikali mwaka 2005/2006 kwa ajili ya uendeshaji wa Mahakama kilikuwa Sh. bilioni 36.6 kwa mwaka huo wa fedha kiasi hicho kimekuwa kikiongezeka mwaka hadi mwaka na kufikia zaidi ya Sh.bilioni 89.9 kwa kipindi cha  mwaka huu  wa fedha.
 “Ongezeko hili ni asilimia 143, kutoka mwaka wa fedha wa 2005/2006  mpaka sasa kutokana na bajeti hii shughuli nyingi za Mahakama zimeboreshwa.’’ alisema.
Jaji Mkuu pia alieleza juu ya ongezeko la rasilimali watu kwa kipindi  hicho  kutoka watumishi 4,972 mpaka kufikia watumishi 6,052 ambao ni ongezeko la watumishi 1080.
 Pia alimpongeza Rais Kikwete kwa kuteua majaji wengi zaidi katika kipindi chake ukilinganisha na majaji waliokuwepo vipindi vitatu vya Serikali iliyopita.
Jaji Mkuu alionge kuwa, kiwango cha usikilizaji mashauri kimeongezeka mwaka hadi mwaka huku mashauri ya muda mrefu yanaharikishwa kwa kufanyika vikao maalum Mahakama Kuu.
 
 Pia katika kipindi hicho, mahakama  hiyo imeweza kuanzisha Mfuko wa Mahakama chini ya sheria ya uendeshaji wa Mahakama namba 4 ya mwaka 2011.
Kwa upande wake Rais Kikwete  wakati akitoa nasaha kwa watumishi wa mahakama hiyo, alisema  mafanikio yamepatikana kwa juhudi za pamoja, yaani Serikali  hiyo pamoja na watumishi hao.
Alisema kuwa, wakati anaingia madarakani kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2005, mahakama  hiyo ilikuwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na bajeti finyu, uhaba wa vitendea kazi, uhaba wa nguvu kazi na mahakama zilikuwa hazitoshi.
“Lakini nafarijika kuwa naondoka kukiwa na mabadiliko makubwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania, ikiwa ni pamoja na kuboresha muundo wa mahakama ambao pia umeongeza rasilimali watu na kuboresha maslahi ya Majaji ili kuwawezesha kufanya kazi kwa bidii,” alisema Rais Kikwete.
Katika hafla hiyo Rais  Kikwete  alikabidhiwa Tuzo na Jaji Mkuu ikiwa ni kumbukumbu ya rekodi aliyoiweka ya mahusiano mema na Mahakama yanayotakiwa kuigwa na awamu zijazo.

No comments:

Post a Comment