Pages

CONTACT

0757092504/0678321772

Sunday, July 17, 2016

WAFANYABIASHARA WA SOKO LA MAILMOJA WAMFAGILIA MSHAMA


indexNa Mwamvua Mwinyi,Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha ,Assumpter Mshama ametaka kuwepo kwa makubaliano baina ya halmashauri ya Mji wa Kibaha na wafanyabishara wa soko kuu la Mailmoja kuhusu kubomolewa kwa soko na kupelekwa eneo la Loliondo.
Amepokea malalamiko juu ya sakata hilo kutoka kwa wafanyabiashara hao ,alipokwenda kuzungumza nao sokoni hapo .
Alisema ni lazima maamuzi yawe yanatolewa kwa kushirikisha walengwa pasipo kuwabana.
Assumpter alitaka kuwepo na makubaliano kati ya pande hizo kwani kunapokuwepo na mazungumzo inakuwa rahisi kufanikisha mambo mbalimbali ya kimaendeleo kuliko kutoa maamuzi ya pande moja.
“Watu mnakaa mnakubaliana kwa pamoja kisha mnatekeleza jambo ambalo tayari limeridhiwa na pande zote mbili, nitakwenda kukutana na viongozi kuzungumza nao kuhusu hili”
“Baada ya kuisikiliza halmashauri nitarudi kuwapatia mrejesho, kwa hapa Kibaha nyie ndio machimbo yetu ya dhahabu hivyo ni lazima tukae pamoja tupange mipango ambayo italeta mwafaka na sio migongano,” alisema Assumpter.
Assumpter alieleza kuwa serikali ya awamu ya tano imelenga kuwatetea watu
wa hali ya chini hivyo akiwa mkuu wa wilaya hataki kuona wanyonge wakinyimwa haki zao.
Alisema atashirikiana nao kutatua changamoto zinazowakabili bila kujali itikadi za kisiasa.
Awali wafanyabiashara katika soko kuu la Mailimoja walitaja changamoto zinazowakabili ikiwemo kutaka kuondolewa kupelekwa Loliondo angali bado taraibu hazikamilika hivyo wanaomba kushirikishwa katika maamuzi yeyote ya kimaendeleo.

Changamoto nyingine kubwa ilikuwa kuhusu uongozi wa soko kukaa madarakani kwa kipindi  cha miaka nane mfululizo.
Zakia Juma alisema mwenyekiti wa soko Ally Gongi (mzee wa shamba)anadaiwa kukaa kwenye nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka minane pasipokufanya uchaguzi wa viongozi, huku akiwa mwenyekiti wa SACCOS ya soko.
Alieleza kuwa kutokuwepo kwa ulinzi sokoni hapo wakati wanalipa ushuru kunasababisha upotevu wa bidhaa na mali zao za kibiashara hivyo kupata hasara .
Hata hivyo wafanyabiashara hao waliomba ridhaa ili wafanye uchaguzi papohapo ambapo mkuu huyo wa wilaya hakupinga,kisha walipendekeza majina ya watu watano ambao walipigiwa kura.
Katika uchaguzi huo Ramadhani Maulid alichaguliwa kuwa mwenyekiti  na hivyo Ally Gongi kukiacha kiti hicho baada ya kukikalia kwa miaka nane.
Nae Gongi alimpongeza Assumpter na kusema katika kipindi
kifupi ameonyesha uchapakazi.
Alisema walikuwa na kero ya dampo ambalo kwa kipindi kifupi cha kuanza uongozi wake limeondolewa kutokana na harufu mbaya iliyokuwepo awali.
Wafanyabiashara sokoni hapo walisema kuwa  wanaikubali serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli na kumuomba Assumpter asichoke kupigania haki zao.

No comments:

Post a Comment