Pages

CONTACT

0757092504/0678321772

Wednesday, July 16, 2014

WACHIMBAJI MADINI WADOGO WAMPONGEZA WAZIRI PROF MUHONGO KUSAFISHA WAPENDA RUSHWA OFISINI KWAKE ,WATAKA WACHIMBAJI WAKUBWA WALIOHODHI MAENEO WAPOKONYWE



Mkuu wa wilaya ya  Iringa Dr  Leticia  Warioba (  waliokaa katikati) akiwa na naibu kamishina  wa madini kanda ya Mbeya Wilfred Machumu na mwenyekiti  wa CCM mkoa wa Iringa Jesca Msambatavangu kushoto katika  picha ya pamoja na wachimbaji  wa madini wadogo mkoa  wa Iringa na Njombe mara  baada ya  kufungua mafunzo ya madini ya  siku tatu  Veta mjini Iringa 




WACHIMBAJI  wadogo  wa madini  mkoani  Iringa  wamempongeza  Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo kwa  kuendelea  kuisuka  upya  wizara  yake  kwa  kuwaondoa  watendaji  waliokuwa  wakifanya kazi kwa misingi ya ubabaishaji  mkubwa  katika  ofisi  za  umma na kutaka kuendelea  kuwaondoa  wale  wote  watakaobainika  kuendekeza rushwa  wakati wa  utoaji wa  vibali .

Wataka  waziri  Prof  Muhongo  kuwatimua kazi  watumishi wake  wasio  waaminifu ambao  wameendelea  kuchochea  migogoro  kwa kuwakumbatia wachimbaji  wakubwa na kuwaacha   wadogo .

Wakizungumza  leokatika warsha ya  siku  tatu ya  wachimbaji  wadogo   inayomalizika  kesho katika  ukumbi wa VETA  mjini  Iringa ,washiriki  hao  akiwemo mwenyekiti wa  wachimbaji  wadogo  Njombe Isaya Mhagama  alisema  kuwa  awali   kabla  ya  wizara  ya  Nishati na madini  haijachukua   hatu ya  kupangua  safu ya  uongozi wa  madini kanda ya  nyanda  za  juu  kusini ,wachimbaji hao  walikuwa  wakinyanyasika na hata  kuzungushwa kupewa  vibali ila kwa  sasa  chini ya  waziri Prof Muhongo hali  hiyo imeanza  kutoweka.

Alisema kuwa  mbali ya  wachimbaji hao  wadogo  kukabiliwa na mitaji katika kuifanya kazi  hiyo ila  bado  ofisi  ya  kamishina  wa madini mikoa ya  kusini  ilikuwa  ikiwajali  zaidi  wachimbaji  wakubwa na hata  kuwanyima  vibali  wachimbaji  wadogo  hali  ambayo kwa  sasa imetoweka  na kubaki tatizo la  mitaji kwa  wachimbaji hao  wadogo .

Hata  hivyo  alisema  kuwa  mara  zote  maeneo ambayo  wanapewa  vibali  wachimbaji  wakubwa ni maeneo ambayo yamegunduliwa na wachimbaji  wadogo  na  kupitia  uwezo wao  wa kifedha  wachimbaji hao  wakubwa  wamekuwa  wakipewa maeneo yaliyogunduliwa na  wachimbaji  wadogo.

Kuhusu  migogoro  kati ya  wachimbaji  wadogo na wakubwa alisema  kuwa migogoro  hiyo  imekuwa  ikichangiwa na  baadhi ya  watumishi wa wizara ya Nishati na madini  ambao  si waaminifu  ambao wamekuwa  wakipokea  rushwa  kutoka kwa  wachimbaji  wakubwa kwa kutumia nafasi yao ya  utoaji leseni ikiwa ni  pamoja na kutoa kwa upendeleo kwa  wenye  fedha pekee.

Pia  walipendekeza  wizara  hiyo kutenga maeneo maalum  kwa ajili ya  wachimbaji  wadogo wa madini ikiwa ni pamoja na  kuwapokonya   maeneo  wachimbaji  wakubwa  ambao  wameshikilia maeneo  makubwa  huku  wachimbaji  wadogo  wakiendelea  kukosa maeneo ya  kuchimba madini huku maeneo hayo makubwa  yakiwa  yamehodhiwa  bila  kuchimbwa .

Mwakilishi  wa ofisi ya madini kanda  ya  Mbeya  Wilfred Machumu alisema  kuwa  ofisi  yake  imeandaa mafunzo  hayo kwa  wachimbaji  hao  wadogo ili  kuweza  kuwapa mwanga wa elimu ya madini na jinsi ya kuifanya kazi hiyo kwa ubora  zaidi.

Hata  hivyo  alisema katika kupunguza malalamiko  ya kukosa   leseni alisema kwa sasa  wapo mbioni kuanzisha utaratibu wa kutumia maombi kwa  njia ya mtandao ili  kukomesha rushwa na malalamiko katika sekta  hiyo.

Pia  alisema katika  kuwafanya  wachimbaji hao  kuboresha  huduma  zao watawapa  elimu ya kuomba mikopo kupitia  benki  na mkopo ambao  wataweza kupata ni kuanzia dola 30,000 kwa  mchimbaji.

  Kwa upande  wake mkuu  wa  mkoa  wa Iringa Dr Christine Ishengoma aliyewakilishwa na mkuu wa  wilaya ya  Iringa Dr  Leticia Warioba alisema kuwa  Serikali iliamua kutunga Sera mpya ya Madini ya Mwaka 2009 yenye kulenga  kuimarisha fungamanisho la sekta ya madini na sekta nyingine za uchumi

Pia kuboresha mazingira ya kiuchumi ya uwekezaji kuongeza manufaa ya sekta ya madini pamoja na  kuboresha mazingira ya kisheria kwa lengo la  kuimarisha uwezo wa Serikali kusimamia sekta ya madini nchini.

" kuwaendeleza wachimbaji wadogo kuhamasisha na kuwezesha uongezaji thamani madini nchini...; na kuimarisha usimamizi wa mazingira"

 Pamoja na malengo hayo alisema kuwa  Serikali itaendelea kuwa msimamizi mwezeshaji na mhamasishaji wa uwekezaji wa sekta binafsi katika sekta ya madini, lakini tofauti na ilivyokuwa huko nyuma (Sera ya madini ya mwaka 1997) kwa sasa Serikali itashiriki kimkakati katika miradi ya madini kwa kupata hisa katika miradi hiyo.
" Naomba nianze kwa kusema kuwa Uchimbaji mdogo kwa muda mrefu umekuwa ukitoa mchango wa uchumi katika  Pato la Taifa kwa kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania pamoja na kupunguza kasi ya vijana kutoka vijijini kuhamia mjini"

  Hata hivyo, mchango wa sekta hii umekuwa ni mdogo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo vifaa duni wanavyovitumia wachimbaji; ukosefu wa maarifa na ujuzi, na ukosefu wa mtaji na teknolojia


HOTUBA YA  MKUU WA MKOA WA IRINGA, MHE. DKT. CHRISTINE ISHENGOMA WAKATI WA KUFUNGUA  MAFUNZO YA WACHIMBAJI WADOGO WA MKOA WA IRINGA TAREHE 16 - 18 JULAI, 2014
Mhe. Mkuu wa Wilaya ya Iringa,
Mhe. Mbunge wa Iringa
Kamishna Msaidizi  wa Madini Kanda ya Kusini Magharibi
Viongozi wa Wilaya ya Iringa,
Maafisa kutoka Wizara ya Nishati na Madini,na taasisi zake,
Watendaji wa Kata na Vijiji mlioko hapa,
Wachimbaji wa madini waalikwa,
Waandishi wa Habari,
Mabibi na Mabwana.
Awali ya yote, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Wizara ya Nishati na Madini kwa kunipa nafasi hii ya kuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa mafunzo ya kuwaelimisha wachimbaji wadogo wa madini wa Mkoa wa Iringa  na baadhi ya viongozi wa Mkoa huu kuhusu usimamizi wa sekta ya madini.  Nitumie fursa hii kuushukuru uongozi wa Wizara hasa ofisi ya Madini Kanda ya Kusini Magharibi kwa kuandaa mafunzo haya na kuyaleta katika Mkoa huu, hususan katika kipindi hiki ambacho shughuli za uchimbaji madini nchini zinakabiliwa na changamoto mbalimbali. Niwashukuru pia kwa kuacha shughuli zenu ambazo ni muhimu kwenu na kukubali kuja kushiriki kwenye mafunzo haya muhimu.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, Kabla ya kufanya kilichotuleta hapa, naomba nianze kwa kusema maneno machache kuhusu sekta ya madini.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, kama wengi wetu tunavyojua kuwa Tanzania imejaaliwa kuwa na hazina ya madini ya aina mbalimbali ikiwemo madini ya metali kama  dhahabu na chuma; madini ya vito vya thamani kama  almasi na tanzanite; madini ya viwandani;  madini ya ujenzi kama kokoto na mchanga; na madini ya nishati kama makaa ya mawe na urani. Kufuatia uwepo wa hazina kubwa ya madini, na kufuatia marekebisho ya kiuchumi yaliyofanywa katika miaka ya 1990, sekta ya madini nayo ilifanyiwa marekebisho ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa Sera ya Madini mwaka 1997 na Sheria ya Madini ya mwaka 1998.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, marekebisho hayo katika sekta ya madini yalivutia kampuni nyingi za uwekezaji katika utafutaji, uchimbaji na kukuza biashara ya madini nchini, hivyo kwa kipindi cha kati mwaka 1997 hadi 2007 mafanikio mbalimbali yaliyopatikana ikiwemo, kuanzishwa kwa migodi mikubwa sita ya dhahabu ambayo ilizalisha wastani wa tani 50;  kuongezeka kwa thamani ya mauzo ya madini nje ya nchi kutoka dola za Marekani milioni 26.66 hadi milioni 1,003.21; kuongezeka kwa ajira kutoka wafanyakazi 1,700 hadi  13,000; na kuongezeka kwa mchango wa sekta ya madini kwenye Pato la Taifa kutoka asilimia 1.4 hadi asilimia 2.7 (kwa bei za mwaka 2001); na kukua kwa sekta ya madini kutoka 7.7% hadi 10.7%
Ndugu washiriki wa Mafunzo, pamoja na mafanikio yaliyopatikana, sekta iliendelea kukabiliwa na changamoto mbalimbali, hususan, kiwango kidogo cha fungamanisho la sekta ya madini na sekta nyingine za uchumi; mchango mdogo katika Pato la Taifa ikilinganishwa na ukuaji wa sekta; kasi ndogo ya uendelezaji wa uchimbaji mdogo; uwezo mdogo wa Serikali kusimamia sekta ya madini; kiwango kidogo cha uongezaji thamani madini; na uharibifu wa mazingira.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, kufuatia changamoto hizo, Serikali iliamua kutunga Sera mpya ya Madini ya Mwaka 2009 yenye kulenga: kuimarisha fungamanisho la sekta ya madini na sekta nyingine za uchumi; kuboresha mazingira ya kiuchumi ya uwekezaji; kuongeza manufaa ya sekta ya madini; kuboresha mazingira ya kisheria; kuimarisha uwezo wa Serikali kusimamia sekta ya madini; kuwaendeleza wachimbaji wadogo; kuhamasisha na kuwezesha uongezaji thamani madini nchini; na kuimarisha usimamizi wa mazingira. Pamoja na malengo hayo, Serikali itaendelea kuwa msimamizi; mwezeshaji; na mhamasishaji wa uwekezaji wa sekta binafsi katika sekta ya madini, lakini tofauti na ilivyokuwa huko nyuma (Sera ya madini ya mwaka 1997) kwa sasa Serikali itashiriki kimkakati katika miradi ya madini kwa kupata hisa katika miradi hiyo.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, Kuhusu kilichotuleta hapa leo hii, Naomba nianze kwa kusema kuwa Uchimbaji mdogo kwa muda mrefu umekuwa ukitoa mchango wa uchumi katika  Pato la Taifa kwa kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania pamoja na kupunguza kasi ya vijana kutoka vijijini kuhamia mjini.  Hata hivyo, mchango wa sekta hii umekuwa ni mdogo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo vifaa duni wanavyovitumia wachimbaji; ukosefu wa maarifa na ujuzi, na ukosefu wa mtaji na teknolojia. Sera ya Madini ya Tanzania inatambua umuhimu na mchango wa uchimbaji mdogo wa madini katika kuinua uchumi.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, kufuatia umuhimu huo mwaka 2006, Wizara ya Nishati na Madini iliandaa mikakati ya kuendeleza uchimbaji mdogo wa madini sambamba na malengo ya MKUKUTA. Pamoja na malengo mengine, mikakati hiyo ya kuendeleza uchimbaji mdogo wa madini imelenga kurahisisha upatikanaji wa vifaa na nyenzo za uchimbaji, kukuza na kuboresha shughuli za uongezaji thamani madini na pia kusaidia vikundi vya wanawake wachimbaji.
Aidha, Kwa kutambua mchango wa uchimbaji mdogo katika Pato la Taifa, na kwa kutambua changamoto walizonazo wachimbaji wadogo, Serikali imefanya juhudi za  kuwaendeleza wachimbaji wadogo wa madini nchini kwa kuwapatia ujuzi na maarifa kwenye nyanja za uchimbaji, uchenjuaji na uongezaji thamani madini; na kuwapatia maeneo ya uchimbaji. Aidha, Serikali imeanzisha Mfuko wa Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo. Katika Semina hii mtafahamishwa fursa zilizopo kupitia mfuko huu.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, nimejulishwa kuwa katika mafunzo haya mtapata uelewa na fursa ya kujadili mada zifuatazo: Sera ya madini, 2009 na Sheria ya Madini ya Mwaka, 2010 na Kanuni zake; Utaratibu wa kupata na kumiliki leseni ndogo za uchimbaji madini na biashara ya madini; Wajibu na Majukumu ya wakala wa ukaguzi wa madini Tanzania, yaani Tanzania Mineral Audit Agency (TMAA); Matumizi ya Hati ya Mauzo ya Madini katika Kusimamia Uzalishaji na Uuzaji madini; Utafutaji na Uchimbaji Salama wa Madini Migodini; Utunzaji wa Mazingira Migodini; Utaratibu wa Upatikanaji, Kumiliki na Utumiaji wa Baruti Katika Uchimbaji Madini; Mafunzo ya Biashara na Ujasiriamali katika shughuli za Madini; Maelezo juu ya Mfuko wa Kuendeleza Uchimbaji Mdogo wa Madini; na Masuala MTAMBUKA (Jinsia, Ajira kwa watoto & Ukimwi)
Ndugu washiriki wa Mafunzo, katika mafunzo haya, mtaelimishwa jinsi Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania unavyosimamia shughuli za uzalishaji na biashara ya madini nchini na jinsi unavyotarajia kuanzisha utaratibu wa kuweka vocha za uzalishaji na biashara ya  madini. Shughuli zinazofanywa na Shirika la madini nchini (STAMICO), ikiwemo masoko. Ninawasihi kusikiliza kwa makini Mada hizo na kushauri ipasavyo ili kazi hiyo iweze kufanyika kwa ufanisi zaidi. Ni matarajio yangu kuwa baada ya kupata uelewa huo, kila mmoja atapata fursa ya kutoa elimu hiyo kwa  wananchi tunaowaongoza kwa upande wa viongozi na wachimbaji kuitoa elimu hiyo kwa wale wanaofanya kazi chini yenu  au wachimbaji wengine ambao hawakupata bahati ya kuhudhuria mafunzo haya.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, ni muhimu kila mmoja wetu kuijua kwa ufasaha Sheria Mpya ya Madini ambayo inatumika katika kuongoza na kusimamia sekta ya madini. Ninatambua kuwa sekta ya madini inakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwa ni pamoja na: (1) leseni za uchimbaji mdogo wa madini kutotolewa kwa wakati; (2) ukosefu wa maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo; (3) suala la fidia ili kupisha, shughuli za migodi, na (4) uharibifu wa mazingira unaosababishwa na shughuli za utafiti na uchimbaji madini. Hivyo, kama watendaji na wasimamizi wa wananchi katika Mkoa huu, ni muhimu kujua vipengele vya sheria vinavyohusika katika kukabiliana na changamoto hizo na kuhakikisha tunazitumia kwa kushirikiana na Maafisa wa Madini ili kuondoa kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wa maeneo yetu. Hivyo, ni matumaini yangu kuwa mtasikiliza na kuchangia Mada hizo kwa umakini mkubwa.
Ndugu washiriki wa Mafunzo, naomba nihitimishe Hotuba yangu kwa kuipongeza sana Wizara ya Nishati na Madini kwa kuandaa mafunzo haya na kuyaleta hapa Iringa. Ni matarajio yangu kuwa elimu tutakayoipata hapa na ushauri tutakaoutoa kwa Wizara husika utasaidia sana katika kuimarisha usimamizi wa sekta ya madini kwa manufaa ya Taifa. Hivyo, niwaombe wote kutumia nafasi hii kujadiliana kwa mtazamo chanya ili kwa pamoja tuhakikishe kwamba sekta ya madini inatoa mchango unaostahili kwenye uchumi.
Baada ya kusema hayo, napenda sasa kutamka kuwa mafunzo haya yamefunguliwa RASMI

ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA

No comments:

Post a Comment